Mpiganaji wa ukweli na kiongozi wa kabila dogo la wahehe aliyetikisa Ujerumani
Hili ni kaburi la Mtwa Munyigumba Kilonge Mdegella
Mwamuyinga lililo katika Kijiji cha Rungemba wilayani Mufindi, takribani
kilometa 61 kutoka Iringa mjini.
Na Daniel Mbega
MAANDIKO kadhaa yamekuwepo kuhusiana na historia ya Wahehe na hasa
ukoo wa Mtwa Mkwavinyika Munyigumba Mwamuyinga, maarufu kama Mkwawa,
lakini yote hayo hayakunizuia kuisaka historia hiyo.
‘Jicho halishibi kuona na Sikio halikinai kusikia!’ hivyo nikaamua
kufunga
safari hadi Lungemba, yaliko makaburi ya Mtwa Munyigumba na ndugu
wengine wa ukoo huo, yapata kilometa 62 kutoka Iringa Mjini.
Wapo walioandika kwamba chimbuko la Mtwa Mkwawa ni Ungazija, lakini
simulizi ninazokutana nazo hapa ni tofauti, maana zinatoka katika vinywa
vya wanaukoo wa Muyinga, ambao nao wameipata ama kurithishwa kutoka
kizazi na kizazi kutokana na simulizi za mababu zao.
Wale waliopata kuandika kwamba asili ya akina Mkwawa ni Ungazija
wanaeleza kuwa mtawala wa Ngazija aliyeitwa Yusuf Hassan ambaye alikuwa
Mwarabu, alizaa watoto wawili wa kiume, Hassan ‘Mbunsungulu’ na Ahmad.
Wanasema kwamba Mufwimi alikuwa mmoja wa watoto watatu wa Mbunsungulu
aliozaa na mwanamke wa Kikaguru. Ndugu zake wengine walikuwa
Ngulusavangi na Ngwila, kwa maelezo yaliyo kwenye baadhi ya maandishi
ambayo inatoweka kutokana na Watanzania kukosa utamaduni wa kutembea,
kujifunza na kudadisi.
Rungemba ni kijiji ambacho hakijasikika sana katika historia kama
lilivyo jina la Mkwawa, lakini hapa ndipo kwa kiasi kikubwa lilipo
chimbuko la Chifu huyo wa kabila la Wahehe na ndipo lilipo kaburi la
Mtwa Munyigumba.
Ignas Pangiligosi Muyinga, maarufu kama Malugila Mwamuyinga (61),
ambaye ni kitukuu wa Msengele Kilekamagana, anaona fahari kuisimulia
historia ya ukoo huo maarufu.
“Shina la ukoo wetu linaanzia kwa mtu aliyeitwa Mufwimi (yaani
Mwindaji), ambaye mababu zetu walitusimulia kwamba alitokea Ethiopia,”
Malugala anaanza kueleza. “Mufwimi alipita akiwinda kutoka Ethiopia,
Kenya kabla ya kuingia Tanganyika na kujikuta yupo Usagara na hatimaye
eneo la Nguluhe-Dabaga akipitia Ikombagulu, himaya ya Chifu Mwamududa.
Wengi walimfananisha na mtu wa kabila la Wakamba kutoka Kenya kutokana
na umbile lake kubwa.”
Wakati huo eneo ambalo sasa linaitwa Iringa lilikuwa na makabila
mbalimbali. Walikuwepo ‘Wahafiwa’ katika Bonde la Milima Welu, Luvango,
Wutinde, Lugulu, Makongati, Kalenga, Kipagala, Kihesa, Tambalang’ombe,
Ibanagosi, Tipingi, Ikolofya, Nyambila, Kibebe na Isanzala.
‘Vanyategeta’ wao walioishi Udzungwa, Kitelewasi na Lundamatwe, ambao
walikuwa wahunzi hodari. ‘Vanyakilwa’ walilowea Mufindi wakitokea
Kilwa; ‘Vasavila’ waliishi milima ya Welu huko Makungu (Kihanga ya
sasa),Magubike na Malangali; na ‘Vadongwe’ waliishi kando ya milima ya
Uhambingeto, Ipogolo, Nyabula na Luhota.
Mufwimi alikuwa mwindaji mkubwa wa nyati ambapo aliichoma nyama yake
kwa kuipaka chumvi ambayo ilikuwa haifahamiki kwa wakazi wa himaya hiyo,
alimpelekea zawadi ya nyama-choma Chifu Mwamududa aliyeipenda mno kwa
ladha yake.
Alipendwa na kukaribishwa na Mwamududa kuishi kwake, lakini
akaanzisha mapenzi ya siri na Semduda, binti wa Chifu huyo, ambaye
alikuwa amewakataa wachumba wengi. Binti huyo akapata ujauzito. Mufwimi
akaogopa kwa kuona amefanya kosa kubwa. Jioni moja akamwita Semduda na
kumweleza kwamba yeye anaondoka, lakini akampa maagizo, ikiwa
atajifungua mtoto wa kike amwite Mng’anzagala na akiwa wa kiume amwite
Muyinga Mufwimi (maana yake ni Mhangaikaji Mwindaji).
Mufwimi alitoroka kwa hofu ya kuuawa na Mwamududa. Akaendelea kuwinda
huko na huko hadi Itamba alikouawa na nyati. Hakuna ajuaye lilipo
kaburi lake.
Lakini kumbe mtawala huyo alifurahi kusikia bintiye ana mimba ya
Mufwimi, maana alijua sasa angekubali kuolewa. Kwa bahati nzuri, binti
huyo alijifungua mtoto wa kiume, hivyo akamwita jina la Muyinga Mufwimi
kama alivyokuwa ameelekezwa na Mufwimi mwenyewe.
“Kijana huyo alipokua, kwa vile Chifu Mwamududa hakuwa na mtoto wa
kiume, akaamua kuukabidhi utawala wake kwa mjukuu ambaye ni Muyinga
Mufwimi aliyekuwa hodari wa vita. Kwa hiyo basi, uchifu huu wa Mkwawa
ulitoka kikeni, na hapo ndipo uchifu ulipoanzia pamoja na ukoo wote
maarufu wa Muyinga,” anafafanua Malugila.
Muyinga Mfwimi akaanza kutawala, akazaa watoto watatu wa kiume –
Maliga, Nyenza na Mpondwa. Mtwa Maliga naye akazaa watoto watano wa
kiume ambao ni Kitova, Mudegela, Mgayavanyi, Mkini na Kigwamumembe.
Inaelezwa kwamba, katika watoto wake hao, alisema Kitova yeye atakuwa
tabibu (mganga wa tiba asilia) na Mudegela atakuwa mtawala, kwa maana
hiyo Kitova alikuwa akitibu maradhi mbalimbali, lakini hasa majeruhi wa
vita na kizazi chake ndicho kinachoendelea kutibu mifupa katika Kijiji
cha Image mpaka sasa.
Mudegela Maliga yeye aliwazaa Lalika, Kalongole, Mbelevele, Wisiko,
Kipaule, Mkanumkole, Lusoko na Mwakisonga. Hata hivyo, uchifu wake
ulikwenda kwa mwanawe wa tano, ambaye ni Mtwa Kilonge.
Kilonge Mudegela alimuoa Maumba Sekindole aliyemzalia Ngawonalupembe
na Munyigumba, lakini pia akamuoa Sekindole mwingine aliyewazaa
Gunyigutalamu, mkewe wa tatu aliyeitwa pia Sekindole aliwazaa Magidanga,
Mhalwike, Mupoma, Magoyo na Magohaganzali.
Hili ni kaburi la Mtwa Msengele Kilekamagana Munyigumba Mwamuyinga, mdogo wake Mtwa Mkwawa kwa Mama Sengimba mdogo. Picha zote na Admin.
“Kilonge alipofariki akazikwa katika eneo ambalo sasa ni Kijiji cha
Lupembe lwa Senga (maana yake Pembe ya Ng’ombe), ambapo kaburi lake
lilikuwa na pembe mbili za tembo, ingawa nasikia pembe zile ziliibwa na
tunaambiwa walioiba wote walikufa ukoo mzima. Nasikia serikali ilipeleka
pembe nyingine na kuzichimbia ili iwe kumbukumbu,” anasimulia Malugala.
Utawala una mambo yake, wakati mwingine unatumia njia halali na
haramu ili kuudumisha. Malugala anasema, Munyigumba, ambaye ni mtoto wa
pili wa Mtwa Kilonge, alihisi kwamba angeweza kuukosa uchifu kwa
kumhofia kaka yake Ngawonalupembe.
“Kwa hiyo akafanya hila na kumuua kaka yake Ngawonalupembe ili yeye
atawale, halafu akamchukua Sekinyaga, mke wa marehemu kaka yake kuwa
mkewe, lakini wakati anamchukua, kumbe tayari Sekinyaga alikuwa
mjamzito.
“Baada ya mtoto kuzaliwa, ambaye alikuwa wa kiume, Mama Sekinyaga
akamwita Malangalila Gamoto, pengine kwa maelekezo ya marehemu
Ngawonalupembe mumewe. Kwa hiyo Malangalila siyo mtoto wa Munyigumba,
bali wa kaka yake ingawa yeye ndiye aliyemlea,” anaeleza Malugala.
Malugala anasimulia kwamba, ugomvi ulitokea baada ya mama huyo
kujifungua ambapo alimwambia Munyigumba kwamba huyu siyo mtoto wake.
Hapo Munyigumba akakasirika na kuamua kumfukuza Sekinyaga na mwanawe.
Inaelezwa kwamba, alipomfukuzwa, Sekinyaga akaelekea katika maeneo ya
Sadani, lakini baadaye Munyigumba akajirudi kwa kuhisi angepata aibu,
hivyo ikabidi amrudishe.
“Sasa wafuasi wake aliowatuma wakamchukue huyo mama wakaenda kumuua
huko Sadani, hata kaburi lake halijulikani liliko. Wao wakarudi na mtoto
Malangalila Gamoto. Kwa hiyo, Malangalila na Mkwawa ni mtu na mdogo
wake kasoro baba zao,” anaeleza.
Munyigumba alikuwa na wake watano – Sengimba, Sendale, Sekinyaga
(aliyekuwa mke wa kaka yake), Sembame na Sengimba mdogo. Sengimba mkubwa
aliwazaa Kilemaganga, Mkwawa, Mpangile, Mulimbila na Wiyolitwe; Sendale
alimzaa Mgungihaka; Sengimba mdogo alimzaa Msengele Kilekamagala;
Sekinyaga alimzaa Malangalila Gamoto (kwa Ngawonalupembe); na Sembame
alimzaa Mpugumoto.