ADVERT 1

ADVERT 1
Kilio na kimbilio la wanahabari Tanzania

Saturday, September 29, 2012

Mhalifu anapopigiwa saluti haki yaweza kupatikana kweli?

KAMANDA wa Polisi wa Mkoa wa Iringa Michael Kamuhanda 

Ninaamini - na ushahidi uko upande wangu - Kamanda Kamuhanda alipaswa kusimamishwa kazi mara moja, kushtakiwa katika mahakama ya kijeshi na kuvuliwa vyeo vyake ili aweze kuunganishwa na watuhumiwa wengine (wale waliompiga Mwangosi wanatakiwa pia wawemo).

KAMANDA wa Polisi wa Mkoa wa Iringa Michael Kamuhanda anastahili kutiwa pingu na kufikishwa mahakamani akiunganishwa na mtuhumiwa nambari moja wa mauaji ya Daud Mwangosi yaliyotokea siku kadhaa zilizopita.

Kushindwa kuchukuwa hatua mara moja dhidi ya Kamuhanda na uongozi wa jeshi hilo na uongozi wa kisiasa nchini ni dalili mbaya zaidi ya kuvunjika kwa mfumo wa utawala wa sheria.

Hili linanikumbusha kisa cha Ukiwaona Ditopile wa Mzuzuri (sasa marehemu) na jinsi uongozi wa kisiasa ulivyojikuta unaweweseka katika kuamua mizani ya haki iende vipi. Hata hivyo, ninaamini kuna sababu kubwa mbili za kwanini kumchukulia hatua Kamanda Kamuhanda kumechelewa, pengine kumetoa nafasi ya kuchezea ushahidi (tampering with evidence), kutishia mashahidi (intimidation of witnesses) na kwa namna yoyote kupindisha mwenendo wa uchunguzi na hivyo kuharibu mchakato wa kupata haki (obstruction of justice).

Kwenye nchi ambayo inaheshimu utawala wa sheria kwa vile Kamanda Kamuhanda alikuwa ni shuhuda wa tukio (material witness) hakupaswa kuwa sehemu ya uchunguzi na kwa hakika hakupaswa kuendelea na wadhifa wake wakati uchunguzi wa mauaji yaliyotokea mbele yake na kwa sababu yake unafanyika.

Kumwacha aendelee na nafasi yake ni mojawapo ya uvunjaji mkubwa wa haki ambao serikali imeruhusu na wanasiasa wetu wanavumilia. Sababu za kwanini Kamuhanda asimamishwe kazi na kufunguliwa mashtaka (asili ya mashtaka sitaki kuhisi sana lakini itakuwa ni kati ya matumizi mbaya ya madaraka hadi mauaji) ni hizi zifuatazo. a. Hakuwa na sababu ya kuvunja shughuli ya Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) ambayo ilikuwa inafanyika kwa mujibu wa sheria.

Kwa wale walioona video ya mazungumzo yaliyotangulia vurumai kati ya Kamuhanda na wandishi wa habari, hoja kubwa ilikuwa kama mkutano wa CHADEMA ulikuwa ni "mkutano wa ndani" (internal meeting) au ulikuwa ni mkutano uliokatazwa.

Wandishi wa habari - hasa marehemu Mwangosi - walisikika wakimpa nafasi nyingi Kamuhanda kubadilisha njia. Kwamba maana ya "internal meeting" si sawasawa na "inside meeting". Kwa maana ya kawaida ya lugha ya Kingereza mkutano unaweza kuwani "internal" bila kuwa "inside". Kwa kauli yake mwenyewe Kamanda Kamuhanda alifanya makosa zaidi pale alipodai kuwa yeye ana haki ya kutafsiri sheria zote na si kipengele kimoja.

Kwa kweli yeye si mtafsiri wa sheria na kama angekuwa na hekima (na ushahidi unaonyesha kuwa hana) alipaswa kuuliza mwanasheria wa serikali au mwanasheria mwingine kama mkutano ule ambao ulikuwa ni "internal meeting" unalindwa na haukuwa sehemu ya mikutano iliyopigwa marufuku. Kwa kutoa agizo la kuuvunja mkutano ule Kamanda Kamuhanda - japo inaweza kuwa ni katika bona fide - alivunja na kuingilia kati shughuli halali ya chama cha siasa kikifanya mambo yake ya ndani.

Hakuwa na mamlaka, wala sababu ya kuingilia mkutano wa ndani na alikuwa na nafasi ya kutosha kuweza kujihakikishia kuwa agizo lake lilikuwa halali.

Kinyume cha watu wengine ambao wanataka kuwa CHADEMA walipaswa kutii amri ya Polisi, binafsi naamini hawakutakiwa kutii amri hiyo ya kuwataka waondoke kwa sababu haikuwa amri halali, haikuwahusu na kwa hakika ilitolewa na mtu ambaye alitumia madaraka yake vibaya.

b. Wakati tukio la kuanza kumpiga mwandishi Mwangosi limeanza Kamanda Kamuhanda alikuwa na haki na uwezo wa kuhakikisha haki za raia zinalindwa.

Polisi wote wanajifunza sheria hii ambayo nimeweka hapo juu ambayo inaelekeza wazi kuwa polisi wanapomkamata mtu au kumzuia mtu asiwatoroke hawapaswi kutumia nguvu zaidi ya inayohitajika.

Yeye kama Kamanda wa Polisi wa Mkoa aliona nguvu ya Jeshi la Polisi iliyokuwapo pale na kwa hakika hakukuwa na mtu hata mmoja ambaye alikuwa ni tishio kwa jeshi hilo. Lakini zaidi ni kuwa walipomkamata Daud Mwangosi hakuwa na kitu kingine chochote cha kutishia polisi zaidi ya kamera na laptop yake. Wingi wa polisi waliomzunguka - picha na video zinashuhudia - unathibitisha pasipo shaka kuwa kama polisi waliamini (kwa sababu yoyote ile) kuwa Mwangosi amefanya kosa na anastahili kuwekwa chini ya ulinzi, polisi walikuwa na uwezo na nguvu ya kuweza kumdhibiti bila kumpiga.

Lakini kwa polisi kumkamata, kumpiga na hatimaye kumuua mbele ya Kamanda wa Polisi wa Mkoa inathibitisha tu kuwa kamanda huyu hafai kuongoza hata chipukizi!

Alitakiwa avuliwe vyeo vyake na kuwekwa kizuizini mara baada ya mauaji yale ya Songea ambayo nayo yalitokea katika mazingira ya kutatanisha. Lakini badala yake magenius wetu wa Taifa wakaona akajaribu kuongoza Jeshi la Polisi kule Iringa.

Pamoja na hayo utaona kuwa hoja yangu inategemea sana kuwa kilichokiukwa ni kifungu hicho cha 21 cha Mwenendo wa Makosa ya Jinai.

Kifungu hicho hata hivyo kinahusiana na tu na pale ambapo polisi wanajaribu kumkatama mtu au kuzuia mtu asiwatoroke. Ukiangalia tukio la mauaji ya Mwangosi ni wazi kuwa kilichotokea ni zaidi ya jaribio la kumuweka mtu kizuizini au chini ya ulinzi.

Mahali ambapo pamezungukwa na polisi wa kila namna na wakiwa na silaha ni mhalifu mjinga kabisa ambaye atajaribu kukimbia au ambaye hatotii amri ya kuambiwa yuko chini ya ulinzi.

Picha za tukio lile zinaonyesha pasi ya shaka kuwa Mwangosi hakuwa kwa namna yoyote ile ni mhalifu anayetaka kukimbia au ambaye ameamuriwa kuwa chini ya ulinzi na akabisha.

Maelezo ya mashuhuda wote waliokuwapo kwenye tukio yanadai kuwa kilichotokea kabla ya mauaji ni Mwangosi kupigwa kwanza na kundi la polisi na kwa dakika kadhaa kabla ya kufyatuliwa bomu.

Kama hili ni kweli – na sidhani kama lina utata sana – mauaji ya Mwangosi yanavuka maelekezo ya Kifungu hicho cha Sheria ya Mwenendo wa Makosa ya Jinai kwa sababu kundi la polisi wakitumia madaraka wasiyo nayo walianza kumpiga raia ambaye hakudaiwa uhalifu wowote na walifanya hivyo mbele ya kiongozi mkuu wa polisi mkoani humo ambaye hakuna mtu hata mmoja aliyejitokeza na kusema kuwa alijaribu kuzuia asipigwe!

Hii inanifanya niamini – na ninaomba msomaji ukubaliane nami – kilichotokea pale ni kitendo cha uhalifu wa ugangwe wa kundi la polisi ambao wakitumia silaha, sare na nafasi zao waliamini wanaweza wakampiga raia yeyote bila kuulizwa.

Na uwepo wa kamanda Kamuhanda pale na ambaye alisababisha mtafaruku ule kwa kutoa amri isiyo halali na kushindwa kwake kuingilia kati kuhakikisha anaokoa maisha ya raia ni dalili kuwa kamanda huyo ni mshirika wa uhalifu (criminal accomplice) na kumwacha aendelee kupigiwa saluti, kushiriki vikao na kuendelea kuongoza Jeshi la Polisi mkoani Iringa ni ucheleweshaji mkubwa wa haki, ni kukejeli akili za Watanzania na kubeza kila namna ya kipimo cha utawala bora. Ni kumlinda mhalifu.

Je atafikishwa mahakamani? Kwa jinsi Polisi walivyochukulia hili na zaidi wanasiasa wetu (wa chama tawala) walivyokubali hili ni wazi kuwa Kamuhanda zaidi atakachofanywa ni kuhamishwa na kupelekwa mkoa mwingine (ningependa binafsi aletwe Dar es Salaam kuchukua nafasi ya Suleiman Kova).

Kumshtaki mtu mkubwa kama huyu ambaye ushahidi dhidi yake ni mkubwa kuliko ule wa Abdallah Zombe na kesi ya wauza madini utatikisa Jeshi la Polisi. Na kwa vile jeshi hili ni la kulindana (IGP Mwema ndiye aliyemuhamisha kutoka Ruvuma!) ni wazi kuwa njia pekee ya kuja kumshughulikia ni uongozi wa CHADEMA kuweka rekodi ya watendaji hawa ili watakapoingia madarakani iwe ni watu wa kwanza kushughulikiwa. Ikumbukwe mauaji hayana muda wa kukoma kuchunguzwa.

Ili kesi hii ionekane ina mfanano wa kudai haki kwa marehemu ni lazima askari wote walioshiriki katika kumpiga marehemu (naweza kujenga hoja kuwa yawezekana walimuua kabla ya bomu kulipuliwa!), baada ya askari mlipuaji bomu kufikishwa mahakamani, sasa afuatie Kamanda Kamuhanda ili kuonyesha kwamba Tanzania kuna mkono wa sheria usio na macho ya upendeleo.

Lakini kwa vile tunajua hili ni gumu kufanyika – kama litafanyika litazungushwa hadi kuondoa maana ya haki – basi Watanzania wajiwekee dhamira kuwa hawa wote waliohusika siku moja watalipishwa.

Na watalipishwa pia wale wengine ambao wataendelea kutoa maisha ya wananchi kwa nguvu ili kujitafutia sifa kwa watawala.

No comments:

Post a Comment