ADVERT 1

ADVERT 1
Kilio na kimbilio la wanahabari Tanzania

Tuesday, September 11, 2012

MAREKANI TENA...............................







Kwa mara nyengine tena Marekani imetangaza kuwa inapinga Palestina kuwa mwanachama kamili katika Umoja wa Mataifa.Victoria Nuland, msemaji wa Wizara ya Mambo ya Nje ya Marekani amesema Washington inapinga juhudi mpya zinazofanywa na Wapalestina za kutaka Palestina itambulike kuwa nchi huru katika Umoja wa Mataifa. 

Siku chache nyuma, Mahmoud Abbas, Rais wa Mamlaka ya Ndani ya Palestina aliwaambia waandishi wa habari huko mjini Ramallah katika Ufukwe wa Magharibi wa Mto Jordan kuwa tarehe 27 ya mwezi huu wa Septemba atawasilisha tena ombi la uanachama wa Palestina katika Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa. Hivi sasa Palestina ni mwanachama mtazamaji tu katika Umoja wa Mataifa asiye na uwezo wa kupiga kura, na matumaini ya viongozi wa Kipalestina ni kuona wanachama wa umoja huo wanaikubali Palestina kuwa mwanachama rasmi na kamili wa Umoja wa Mataifa.

 Ombi la kutaka kutambuliwa rasmi nchi huru ya Palestina mji mkuu wake ukiwa ni Baitul Muqaddas liliwasilishwa na Mahmoud Abbas kwa Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Ban Ki-moon, lakini halikupasishwa kutokana na uungaji mkono wa kila hali wa Marekani kwa utawala wa Kizayuni wa Israel, pingamizi za Washington ndani ya Umoja wa Mataifa pamoja na msimamo dhaifu wa maafisa wa umoja huo. Hadi sasa karibu nchi 140 zimetangaza kuwa zinaunga mkono mpango wa kuundwa nchi huru ya Palestina. Katika miezi ya hivi karibuni Wapalestina wameanzisha kampeni kubwa kwa lengo la kutaka Palestina itambuliwe kuwa nchi huru na Umoja wa Mataifa, na juhudi hizo za Wapalestina kupigania haki yao hiyo zimepata uungaji mkono mkubwa kimataifa. 

Lakini hayo yanajiri katika hali ambayo katika kuendeleza upinzani wake kwa juhudi hizo za kuhakikisha Wapalestina wanapata haki zao ikiwemo kuunda nchi yao huru, Marekani inaweka vikwazo na pingamizi ili kufelisha na kukwamisha tena juhudi za Wapalestina za kutaka kutangazwa kuundwa nchi huru ya Palestina katika Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa mnamo mwishoni mwa mwezi huu. Marekani ndiyo nchi pekee inayopinga suala hilo, ambapo kwa kutumia kila aina ya mbinu zikiwemo za kutishia kutumia kura yake ya veto dhidi ya ombi la Wapalestina katika Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa imeviza na kufelisha juhudi za Wapalestina za kutaka Baraza la Usalama lipasishe azimio la kutambuliwa rasmi nchi huru ya Palestina. Vizuizi na pingamizi hizo za Marekani zinakinzana kikamilifu na maazimio yaliyopasishwa na Umoja wa Mataifa ambayo yanaunga mkono na kutilia mkazo haki za Wapalestina kujiamulia mustakabali wao na kuwa na nchi yao huru. 

Kuhusiana na nukta hiyo mwaka 2010 Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa lilipitisha kwa wingi mkubwa wa kura azimio la kuunga mkono haki ya taifa la Palestina kujiamulia mustakabali wake. Azimio hilo lilisisitiza na kutilia mkazo kwa mara nyengine tena haki ya wananchi wa Palestina kuamua juu ya mustakabali wao ikiwemo kuwa na nchi yao huru.

 Pamoja na hayo hatua hiyo iliyochukuliwa na Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa na uungaji mkono wa nchi nyingi duniani kwa haki za taifa la Palestina umekosolewa na kulaumiwa na Marekani, ambayo ndiyo muungaji mkono mkuu wa utawala wa Kizayuni wa Israel, kitendo ambacho kinadhihirisha upeo wa juu kabisa wa uadui wa Washington kwa wananchi madhulumu wa Palestina

No comments:

Post a Comment