ADVERT 1

ADVERT 1
Kilio na kimbilio la wanahabari Tanzania

Friday, September 28, 2012

TATIZO HILI LA KAZAGAA KWA TAKA IRINGA VIONGOZI MNAONA? AU BADO MPO MPO KWANZA?

(Story kwa hisani ya Francisgodwin.blogspot.com) 
 
hapa ni kata ya kweakilosa eneo la kota za polisi taka zikiwa zimejazana barabarani
Hizi ni takataka zilizojaachwa bila kutolewa katika kata ya Ilala kata anayotoka naibu meya wa Manispaa ya Iringa Grevas Ndaki
uchafu huu ukiwa umezagaa kota za polisi Frelimo baada ya Manispaa ya Iringa kushindwa kutoa taka zilizomwangwa na wananchi katika kituo cha taka eneo hilo
Hapa ni Ilala taka zikiwa zimemwangwa nje ya nyumba ya mtu.
Mkurugenzi wa Halmashauri ya Manispaa ya Iringa Teresia Mahongo
Mwandishi wa makala  haya Bw Fredrick Jailos anaanza kwa  kuhoji  kuwa , Tumekosea Wapi?Tatizo la kuzagaa kwa taka taka katika Manispaa ya Iringa mkoa wetu wa Iringa linakua kwa kasi kila siku.
hili licha ya kua linaharibu sifa na hadhi ya mkoa wetu kama moja ya mikoa misafi Tanzania, pia linahatarisha maisha ya viumbe hai - binadamu, mimea, wanyama na viumbe vidogo kabisa (micro-organisms) Sifa ya usafi kwa mkoa wa Iringa imedumu kwa miaka kadhaa, lakini kwa hali ilivyo sasa, yawezekana sifa hiyo ikapotea.
Miaka kadhaa iliyopita, Iringa kulikua na makontena makubwa kwa ajili ya kuhifadhia taka katika mitaa. Baada ya siku mbili tatu, gari lilipita kubeba makontena hayo na kwenda kumwaga uchafu katika dampo la manispaa.
kontena lilirudishwa sehemu ile ile na wananchi wakaendelea kulitumia kuhifadhi taka! Tatizo la kuzagaa kwa uchafu katika mitaa mbalimbali ya mkoa wa Iringa kwa kiasi kikubwa lilipungua, na mji kuonekana msafi kwa muda mwingi.
Zaidi ya makontena hayo, kuna baadhi ya mitaa ilijengewa vizimba kwa ajili ya kuhifadhi takataka.Vizimba hivyo viliwezesha uchafu wa aina tofauti kuhifadhiwa hapo mpaka siku ambayo gari itapita na kuukusanya.
 Kwa hali ya sasa, vizimba hivyo vimekua vikiachwa kwa muda mrefu bila kuondolewa takataka zilizorundikana ndani yake hivyo kusababisha usumbufu kwa jamii zinazoishi karibu kabisa na vizimba kwani uchafu huo hutoa harufu na kusambaa eneo lote la makazi
. Unapopita katika mitaa ya Iringa leo hii, utakuta hali tofauti! Makontena mengi hayapo kwenye maeneo yaliyokuwepo na kusababisha wananchi kutupa taka chini! Makontena ambayo yamebaki katika baadhi ya maeneo hayatolewi mara kwa mara kwa ajili ya kwenda kumwagwa uchafu kama ilivyokua zamani.
 Hali hii inasababisha makontena hayo kujaa kupita kiasi, mpaka inafikia hatua wananchi wanamwaga taka taka chini. Takataka hizo hukaa hapo kwa muda mrefu mpaka kuja kutolewa.
Uwepo wa takataka hizo sehemu moja kwa muda mrefu husababisha harufu mbaya katika eneo husika, na harufu hiyo husafiri mpaka kufikia umbali wa mita 200 kutoka sehemu yenye uchafu.
Taka taka za plastiki, karatasi na chupa pia zinasafirishwa na upepo, maji yanayotembea, na shughuli za binadamu kufikia mpaka umbali wa zaidi ya mita 500 na kwenda kuchafua mazingira ya mitaa au maeneo mengine.
Ingawa kwa kiasi kidogo, lakini kuna taka za sumu (kemikali) zinazotupwa katika vizimba na makontena yaliyoko sehemu za makazi (mf. Makopo ya kemikali zinazotumika katika saluni za kiume na za kike).
Taka taka za namna hii zikikutana na jua na maji husababisha mmenyuko wa kemikali (chemical reaction), na kupelekea uharibifu wa mazingira! Pia, takataka za kemikali zinaweza kusafiri umbali mrefu ndani/chini ya ardhi na kusababisha eneo kubwa kuathirika. Tatizo hili yawezekana linasababishwa na mambo yafuatayo:
I. Ukosefu wa sheria ndogo ndogo zinazosimamiwa vizuri katika suala la uhifadhi wa taka.
II. Upungufu wa mapipa madogo ya kuhifadhia takataka katika mitaa mbalimbali ya mkoa wa Iringa.
III. Ongezeko la idadi ya watu wanaoishi ndani ya manispaa – hii imesababisha kuongezeka kwa matumizi ya vitu/vifaa mbalimbali na kuongeza wingi wa taka taka zinazozalishwa kwa siku.
IV. Kuchakaa kwa baadhi ya makontena ya kuhifadhia uchafu, pia kubomoka kwa vizimba. Hii imesababisha upungufu wa vifaa hivyo, na kuwalazimu wananchi katika baadhi ya mitaa kumwaga taka taka chini.
V. Ukosefu wa elimu ya mazingira kwa wananchi wa kawaida na kupelekea matumizi mabaya ya vizimba na makontena ya kuhifadhia taka.
VI. Kutokua na utaratibu na usimamizi mzuri wa vizimba na makontena ya kuhifadhia uchafu.
\VII. Ratiba ya gari ya kuzoa taka haiko
wazi na haieleweki. Pia, kuna upungufu wa magari ya kufanya kazi hii.
VIII. Uzembe wa baadhi ya watendaji wa manispaa katika kusimamia suala la udhibiti wa taka.
NI NIN ATHARI ZA TAKATAKA HIZI. a. Uharibifu na Uchafuzi wa Mazingira. b. Kusababisha magonjwa ya mlipuko. c. Kuharibu sifa na mandhari ya mji. d. Kupunguza uwezo wa uzalishaji wa ardhi (rutuba) e. Kuchochea ukuaji au mazalia ya vimelea vya magonjwa kwa wanyama na mimea mingine.
NINI KIFANYIKE? Kiujumla, suala la uhifadhi na usimamizi wa taka ni suala linalohitaji pesa na maandalizi ya kutosha. Lakini kuna ulazima wa suala hili kupewa uzito unaostahili ili Iringa, wananchi wake na viumbe wengine waendelee kuwa salama. Baadhi ya mambo yanayoweza kusaidia kupunguza tatizo hili ni pamoja na;
 i. Kuwe na sheria ndogo zinazosimamiwa vizuri za uhifadhi wa taka katika maeneo ya mjini. Sheria hizo zaweza kuwa sawa au zinazofanana na zile zinazotumiwa katika mkoa wa Kilimanjaro katika uhifadhi wa taka (Kwa Mkoa wa Kilimanjaro, ni marufuku kutupa taka taka hovyo, na hilo linazingatiwa na wananchi kwani kuna usimamizi mzuri wa sharia hiyo ndogo)
 ii. Kuna haja ya kutafuta makontena zaidi na kuyaweka katika maeneo mengi zaidi. Kutokana na kuongezeka kwa kasi kwa idadi ya watu mkoani Iringa (kukichangiwa na uwepo wa vyuo vikuu vitatu), kuna haja ya kuongeza idadi ya vizimba na makontena katika kila mtaa wa manispaa yetu.
 iii. Elimu ya uhifadhi wa taka itolewe kwa wananchi wa kawaida. Serikali ya mkoa kwa kushirikiana na wadau wengine wa mazingira mkoani Iringa (na kwingine) iandae mafunzo ya elimu ya uhifadhi wa taka kwa ngazi ya kata na mitaa (wenyeviti, watendaji, mabalozi nk.). Elimu hii inaweza kutolewa kwa viongozi wa kata na mitaa. Viongozi hao wawajibike kuifikisha elimu hii kwa wananchi wa sehemu zao.
 iv. Ushirikishwaji wa wadau wa mazingira katika program ndogo ndogo ni muhimu. Kwa Mfano EBONY FM wamewahi kuwa na shughuli za kuchangisha pesa kwa ajili ya kununua mapipa ya takataka kwa ajili ya mitaa ya Iringa mjini. Wadau zaidi wakipewa mwamko, kutakuwa na unafuu kwa kiasi kikukwa.
v. Ratiba ya gari ya kubeba taka iwekwe wazi kwa viongozi wa kata/mitaa ili kupunguza tatizo la vizimba na makontena kujaa kupita kiasi.Kuwepo na ratiba ya wazi kwa wananchi kuhusu siku za kukusanya takataka kwenye mitaa. Kwa kila kizimba au mtaa, ziwepo siku maalumu za kukusanya taka, na wananchi wa maeneo husika waambiwe siku hizo. Kwa kufanya hiyo itasaidia katika kutoa taarifa pale gari ya kutoa takataka itakaposhindwa kufika katika mtaa. Pia, inaweza kusaidia kwa wananchi kujipangia utaratibu wa kupeleka taka katika vizimba na makontena.
 vi. Kuna haja ya kuongeza gari za kuzolea taka ndani ya manispaa. Hii inaweza kufanyika kwa manispaa kununua gari zaidi, au kutoa zabuni kwa makampuni binafsi kwa ajili ya kazi hii.
vii. Kuna haja ya kuwa na mafunzo ya uhifadhi wa mazingira mashuleni. Zaidi ya mitaala ya elimu inayozungumzia uhifadhi na usimamizi wa mazingira, manispaa (kupitia idara au kitendo kinachojihusisha na usimamizi na uhifadhi wa mazingira) wanaweza kuandaa program maalum ya kupita mashuleni na kutoa elimu na mafunzo kuhusu uhifadhi wa taka. Kwa njia hii, kaya nyingi za mitaa mingi zitafikiwa kiurahisi. Program hii ihusishe shule za misingi na sekondari.
viii. Manispaa iwe na mtu/watu maalumu, ambaye ni mtaalamu wa mazingira kwa ajili ya kuratibu na kusimamia shughuli za uhifadhi wa taka tu. Mtu huyo anaweza kutoka katika kitengo cha mazingira au kuajiliwa. Kwa kuwa na watu wa namna hiyo, itakuwa ni rahisi kufahamu hali ya mkoa wetu, na pia kuwajibishana pale inapobidi.
ix. Utaratibu wa watu kupita nyumba kwa nyumba kukusanya uchafu mara moja au mbili kwa wiki utasaidia kupunguza tatizo hili. Kila kaya itatakiwa kuhifadhi taka taka zake, mpaka siku ambayo timu itapita kuukusanya na kwenda kuutupa sehemu husika.
Kwa huduma hii, kila familia itatakiwa kulipia kiwango cha pesa kitakachokubaliwa (mf. Tshs 500/ kwa kila familia). Hitimisho Miaka kadhaa iliyopita Iringa ilikuwa inasifika kama mkoa msafi zaidi Tanzania. Lakini kwa sasa hatupo tena kwenye nafasi hiyo.
Na hata kama tunaingia kwenye mikoa mitatu misafi zaidi nchini, hatustahili kuwepo kwenye nafasi hiyo kwani hali yetu ni mbaya(Ingawa walioko nyuma yetu wana hali mbaya zaidi). Tuna vichache vya kujivunia katika suala la uhifadhi wa mazingira, alkini juhudi zaidi zinahitajika ili kuurudisha mkoa kwenye heshima yake ya awali.
 Tuangali tulipokosea na tujisahihishe kabla kipindupindu na magonjwa mengine ya mlipuko hayajatushambulia. Ingawa jukumu hili linaonekana kuwa la uongozi wa manispaa zaidi, lakini wananchi wanahusika kwa kiasi kikubwa kulifanikisha hili.
 Ushirikishwaji wa wananchi na wadau wengine (vyombo vya habari, AZAKI, NK) katika uhifadhi wa taka, kuanzia ngazi ya kaya utasaidia kupunguza tatizo hili kwa kiasi kikubwa. Hivyo basi, kuna haja ya manispaa kujipanga upya katika mpango wake wa uhifadhi wa taka na kutia nguvu zaidi sehemu zenye mapungufu. Tumepotea njia, ytunakoenda ni kule tulipotoka miaka mingi iliyopita.
Hatua inayofuata ni kujipanga upya na kutafuta njia sahihi ya kutufikisha tulipokuwa tunatakiwa kwenda. Mazingira safi na salama ni haki ya kila mmoja wetu. Hivyo ni wajibu wa kila mwana Iringa kuhakikisha kuwa anawajibika kuhifadhi mazingira hayo.
 Na ili wajibu huu uwe sahihi, wananchi wafundishwe/waelekezwe ni nini wanatakiwa kufanya ili tuendelee na safari kuelekea kwenye sifa ya mji wenye mazingira safi na salama zaidi Tanzania.


mkazi wa Frelimo akitoka kutupa taka kata eneo hilo hilo ambalo taka zimezagaa
Kwa  hali  hii  uongozi  wa Manispaa ya Iringa akiwemo  mbunge mchungaji Peter Msigwa na  wabunge  wa viti maalum Ritta kabati  (CCM) na Chiku Abwao (chadema) sasa  wanapaswa  kuendelea  kuimba  wimbo  wa usafi katika mji  wa Iringa .

Haitoshi kwa  viongozi hao  wa kisiasa  pia mkuu  wa mkoa  wa Iringa Dkt Ishengoma na katibu tawala Bi Mpaka  pamoja na mkuu  wa wilaya ya Iringa Dkt Warioba ambao kimsingi ni  wakazi  wa Manispaa ya Iringa hawana sababu ya  kuendelea  kuzichekea  takataka  hizo wanapaswa  kushirikiana na mkurugenzi wa Manispaa ya Iringa na madiwani  wa kata zote  kuzichukia na kuzishughulikia vinginevyo mkoa  wa Iringa utaongoza kwa aibu kwa ajili ya Manispaa ya Iringa .

No comments:

Post a Comment