FARM INPUT PROMOTION’s
AFRICA
- FIPS Africa Mkombozi wa mkulima mdogo vijijini
Wakulima kutoka katika wilaya ya Kongwa,Kilombero,Mvomero na
Kiteto wakifuatilia kwa karibu mafunzo ya wakulima wakufunzi ngazi ya kijiji
(VBAA)
“Mmekuwa mkilima kwa muda mrefu
bila kupata mafanikio kutokana na kulima kilimo cha mazoea lakini sasa kupitia
kwa maafisa ugani wa mradi mmefundishwa mbinu bora za kilimo na matumizi
ya mbolea na mbegu za kisasa zitakazoongeza uzalishaji” Hayo yalisemwa na ndugu
Abel Mngale Meneja katika mradi wa Nafaka wakati akifungua mafunzo ya siku tatu
kwa wakulima kutoka katika wilaya za kongwa, kiteto,Kilombero na Mvomero katika
chuo cha LITI mkoani Morogoro mwishoni mwa wiki
iliyopita.
FIPS Africa ni taasisi isiyo ya
kiserikali chini ya ufadhili wa serikali ya watu wa Marekani katika kupunguza
umasikini na kuongeza uzalishaji wa
mazao ya chakula na lishe
Mafunzo hayo yaliyoshirikisha
watoa mada kutoka Wizara ya Kilimo na Chakula,wadau kutoka makampuni ya mbolea
na mbegu na watafiti wa mazao kutoka katika vituo vya kilimo vilivyopo nchini
katika kuhakikisha kuwa wakulima wahamasishaji 107 kutoka wilaya hizo
wanapatiwa mafunzo ya kuwa mawakala na wasambazaji wa mbolea na mbegu katika
ngazi ya vijiji ili kuweza kuwafikia wakulima wengi na kuwapunguzia gharama za
usafiri kufuata mawakala wa mbegu.
“Mbinu husishi za kuboresha na
kuhifadhi rutuba ya udongo zinajumuisha matumizi ya mchanganyiko wa vyanzo
mbalimbali vya kurutubisha udongo ambavyo wakulima mnao uwezo wa kuvipata kwa urahisi na vinapatikana
kwenye mazingira yane, kama vile mbolea za asili na zile za viwandani” alisema
Dr Choloba Mkangwa mtoa mada kutoka chuo cha utafiti Ilonga- Kilosa Mkoani hapa .
Aidha wakala mhamasishaji kutoka wilaya ya
Mvomero ndugu Hassan Songoro aliuomba mradi na serikali kwa ujumla kuhakikisha
kuwa pembejeo za kilimo zinawafikia wakulima katika wakati unaofaa ili kuendana
na msimu wa upandaji kwani wamekuwa wakiletewa mbegu kwa kuchelewa.
Akifunga mafunzo hayo DALDO wa wilaya ya Kongwa aliwapongeza wakulima wahamasishaji hao kwa kuitikia wito wa kuhudhuria mafunzo
hayo yatakayowapa fursa ya kuwa mawakala wa pembejeo za kilimo vijijini ili
kupunguza mzigo kwa wakulima wenye kipato kidogo kupata pembejeo za kilimo kwa
urahisi.
No comments:
Post a Comment