BAADHI YA MISEMO NA METHALI TOKA TANZANIA
1. Acha kukuna makovu ya mende (Kichaga)
Maana yake
ni kwamba uache kukumbuka taabu ya wakati uliopita. Methali hii
itafahamika vizuri kama tukielewa kwamba hapo zamani katika jamii zetu,
mende walikuwa wanaonekana kwa wingi katika nyumba. Nao mende ni hodari
wa kuuma watu wakati wa usiku wakiwa wamelala. Na pale walipouma hubaki
kovu ambalo hukuna. Lakini pia ambaye ameshaumwa na mende hao itakuwa ni
kazi bure kama atakalia kuyakuna makovu hayo.
Methali hii hutumika kwa kuwaonya watu wasikalie kufikiria makosa au taabu za wakati uliopita.
2. Afadhali kuchakaza nguo kuliko akili (Kipare)
Maana
yake ni kuwa hakuna kitu bora kama akili (hekima). Mtu ambaye hana
hekima ya uchi kuliko uchi wa aina yoyote ile. Kuwa uchi kinguo, mtu
anaweza kununua zingine. Lakini mtu anapokuwa uchi kiakili, hakuna
maarifa.
Methali hii hutumika kwa kumhurumia mtu ambaye ameharibikiwa na akili na anafanya majambo isivyotakiwa katika jamii.
3. Amekufa hata Mwakafwile aliacha mwana alipokufa (Kinyakyusa)
Methali
hii inatokana na mila za kibantu kukosa mrithi ni mwisho wa ukoo na
jina la ukoo. Mtoto wa kiume huendeleza ukoo. Ni jambo la kusikitisha
sana kutokuwa na mwana mrithi.
Maana ya methali hii ni kwamba mtu anayehusika hana msaada wowote kutoka kwa ndugu, jirani au mahali penginepo.
Hutumika
na mtu binafsi aliyezama ndani ya kilindi kikubwa cha matatizo, wala
hana mtoto au mtu wa karibu naye ambaye angeweza kumsaidia. Ni methali
ya watu maskini na wanyonge katika kuhurumiana shidani. Kama kuunguliwa
nyumba, kufiwa nk.
4. Anayetaka usawa mwisho wake uchawi (Kikerewe)
Methali
hii ina maana kwamba tukubali kuwa binadamu budi kutofautiana. Fulani
kapata baiskeli – lazima nami nipate, fulani kapata nyumba – lazima nami
nipate nk. Maneno kama haya mwishowe humsukuma mtu kutumia hila mbaya
au njia zisizo za kawaida kama vile uchawi.
Methali hii hutumika katika kuwaonya wanopenda kujikweza.
5.Fimbo ya jirani haiui nyoka (Kiiraqw)
Ujirani
ni jambo jema lakini si vizuri kutegemea misaada yote toka kwa
majirani. Methali hii inafundisha umuhimu wa kujitegemea na si kutazamia
kupata misaada kila uhitajipo.Pia, ni lazima ieleweke kwamba hakuna
sheria inayomfanya jirani atoe msaada hata kama anaweza, yote hutegemea
matakwa yake na huwezi kubashiri ni lini atakataa kutoa msaada.
6. Fungo alikosa mkia kwa kulala (Kizigua na kinguu)
Ipo
hadithi katika hadithi za Kizigua na Kinguu isemayo kuwa kwa sababu ya
usingizi wake Fungo alikosa au aliupoteza mkia wake. Methali hii
inaonyesha hasara ya uzembe na kuchelewa mara nyingi. Hali hii inaweza
kumkosesha mtu mambo mengi mazuri au kupoteza maslahi yake ambayo
yangemfaa baadaye. Hutumika kama onyo kwa wazembe.
7. Anayelala na mgonjwa ndiye anayejua miugulio (Kisambaa)
Maana
yake ni kwamba huwezi kujua undani wa mtu mpaka uwe naye karibu katika
uhusiano. Hutumika kwa mtu anayejitia kujua sana mambo ya ndani ya
wengine kuliko wenyewe wanaohusika.
8. Hohehahe hakosi siku yake (Kiha)
Maana
yake ni kuwa kila mtu ana bahati yake. Hata maskini ana siku yake ya
bahati. Hutumika kama onyo kuwa inafaa kuthamini watu kwa utu wao na
wala si kwa mali walizonazo. Mtu ni utu.
9. Kondoo wa madoadoa hawako katika jamii ya wanadamu (Kimasai)
Wanadamu
wote hawahitilafiani sana kwa maumbile yao, na ndio maana tunaweza
kusema, binadamu wote ni sawa. Tusikiapo kitu kisicho cha kawaida kuhusu
mtu tunaweza kutumia msemo huu kumaanisha kwamba tumestaajabishwa na
habari hizo. Msemo huu unatumika pia katika kukanusha habari
zisizoaminika.
10. Kucheka chongo ya mwenzio na hali yako umefunika (Kisukuma)
Maana
yake ni kuwa si vizuri kucheka makosa ya wengine kwani huenda ukafanya
makosa yale yale na pengine una udhaifu wako ambao wengine wanakucheka.
Hutumika katika kuwaonya watu wanaocheka dosari au udhaifu wa watu
wengine na pengine watu wanaocheka wenzao waliopatwa na maafa k.m.
kufilisika.
11. Mbwa mwenye mnofu mdomoni hapigi kelele
(Kifipa) Maana yake ni kama methali ya kiswahili isemayo:- Mwenye shibe
hamjui mwenye njaa. Methali hii hutumiwa kwa kuwasema watu ambao wana
kitu na huwasahau wale ambao hawana kitu. Zaidi, huweza kutumika kwa
kuwaonya viongozi wanaosahau kuwatetea wenzao baada ya kupata madaraka
na shibe.
12. Mwenda usiku amesifiwa kulipokucha
(Kikwere) Mwenda usiku hapa ni sawa na mtu ayetenda jambo ambalo kwa
wakati ule wengine hawalielewi. Lakini mwishowe jambo hilo lilipoonyesha
mafanikio ndipo watu wakaanza kumsifu. Hutumika kwa mtu anayechekwa na
wenziwe juu ya jambo alitendalo iwapo wakati ule wale wamchekeo
hawaelewi usahihi wa lile alitendalo.
13. Nguo ya mzee haikosi chawa
(kimeru) Maana yake, mzee hakosi akiba. Maana ya methali hii
itafahamika zaidi si kwa vile hali ya uchafu ndiyo iletayo chawa, bali
kwamba kwa mzee huwa na akiba za aina aina nayo maana yake ni ile nzuri.
Methali hii hutumika wakati mtu anapozungumzia utajiri wa mtu mzee. Ni
kama njia ya kuwakoga wengine kwamba wakati wote utazamie kumkuta mzee
katka hali nzuri, anayo akiba yake ambayo ameihifadhi.
14. Usidharau wakunga uzazi ungalipo
(Kibena) Wakunga ni watu wenye kuheshimiwa sana kwa sababu ya ufundi na
ujuzi wao wakati wa kuzalisha. Kwa kuchukua umuhimu wao huo, wanawake
hushauriwa kutowadharau maadamu wangali wanazaa, isijeikawa wakti wa
kujifungua wakakosa msaada. Matumizi ya methali hii ni kuwaonya watu kwa
ujumla wasiwe na dharau kwa kitu ambacho kitawafaa katika maisha yao.
Zaidi kwamba, kitu kilichokusaidi wakati uliopita usikidharau kwa vile
hukitumii kwa wakati huu.